Dec 19, 2011

UGONJWA WA FACEBOOK

Watumiaji wa mtandao wa jamii wa Facebook wameonywa juu ya kuibuka kwa ugonjwa mpya wa ulevi wa mtandao huo.  Ugonjwa huo mpya unajulikana kitaalamu kama Facebook Addiction Disorder (FAD).
Mtaalamu wa saikolojia  Dr. Michael Fenichel, ambaye ametoa machapisho kadhaa kuhusu FAD mtandaoni, ameelezea dalili za ugonjwa huo ni pale mtumiaji anapoipa kipaumbele Facebook kuliko shughuli zingine za kila siku kama kuamka, kula, kutumia simu kwa matumizi mengine ama kusoma barua pepe zingine.
"Jambo la kustaabisha ni kuwa, kama ilivyo kwa simu za mikononi, hakuna mtu anayegundua juu ya muda na nguvu inayopotea kazini na majumbani.  Sasa hata watu watembeapo, wamejitolea muda wao kwa ajili ya Facebook.”   Dr.  Fenichel aliyazungumza hayo katika chapisho la mtandaoni juu ya changamoto mpya kutokana na FAD.
FAD inaweza pia kuelezwa kama ulevi kupindukia wa tarakilishi.

Jitambue kuwa na ugonjwa huo endapo...
Kwa mujibu wa  Joanna Lipari,  mtaalamu wa saikolojia ya tiba kutoka Chuo Kikuu cha California, Los Angeles alipohojiwa na CNN report, hizi ni dalili kama unaugua ugonjwa wa FAD
1. Unapoteza usingizi kwa ajili ya Facebook. Matumizi ya Facebook yanapokuwa ya lazima kwako kiasi cha kuwa logged in usiku kucha, matokeo yake ni kushinda mchovu siku nzima ifuatayo.
2. Unatumia zaidi ya saa moja ukiwa  Facebook. Lipari alisema ni vigumu kusema ni kiasi gani kiasi kikubwa cha matumizi ya Facebook, lakini kwa wastani mtu anapaswa kutumia chini ya nusu saa kwa siku akiwa Facebook.
3. Unaanza kuzoweana na kuwa karibu na wapenzi wako wa zamani uliokutana nao Facebook.
4. Unadharau kazi kwa ajili ya Facebook. Hii inamaanisha unautumia muda mwingi Facebook kuliko kutimiza majukumu yako ya kazi..
5. Mawazo juu ya Facebook yanakuacha katika wahka. Ikitokea ukaikosa Facebook unapatwa na mfadhaiko, wasiwasi ama dukuduku.  Hii inaashiria unahitaji msaada wa haraka sana.
Wataalamu wa tiba huko Marekani wamekutana na ongezeko la wagonjwa wanaokabiliwa na athari za mitandao ya jamii, ikiwa ni pamoja na kutofanya kazi ama kukosa hamu ya mapenzi.
Facebook
Facebook, iliyoanzishwa na bilionea mdogo zaidi ulimwenguni Mark Zuckerberg, ina watumiaji zaidi ya milioni 500 kote ulimwenguni, nusu yao huingia Facebook kila siku. Idadi ambayo kama ingekuwa ni nchi, basi ingekuwa ya tatu duniani kwa idadi ya watu baada ya China na India.
Kuna picha zaidi ya bilioni 2, huku video zikiwa zaidi ya milioni 14 katika kurasa mbalimbali za Facebook.  Takribani sekunde zipatazo bilioni 6 hutumiwa ndani ya Facebook kila siku, kote ulimwenguni.
Kwa mujibu wa Willis Wee, mwanzilishi wa blog ya habari za jamii na masoko ya Penn-Olson.com, idadi hii ni zaidi ya mara mbili ya idadi ya watumiaji wa mtandao maarufu wa utafutaji wa Google.

No comments:

Post a Comment